Uchanguzi CCM Zanzibar manun’uniko kila kono

Uchanguzi CCM Zanzibar manun’uniko kila kono

Photo: Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ, Mhe. Haji Omar Kheri Akiwasilisha Bajeti ya Wizara yake.

Na Mwandishi Wetu

Uchaguzi ndani ya Chama cha Mapinduzi kwa upande wa Zanzibar umetawaliwa na vituko na ukiukwaji wa taratibu katika Mikoa kadhaa Kichama.

Katika Mkoa wa Magharibi Kichama, sanduku la kura liliibwa huku idadi ya wajumbe waliopiga kura wakiongezeka kinyume na wale waliokuwepo kwenye ukumbi waliohudhuria mkutano wa Uchaguzi.

” Uchaguzi wetu ulitawaliwa na mazonge mengi, kwa mfano mjumbe mmoja Marehemu Dkt Mwinyihaji Makame ni marehemu,lakini kura yake imepigwa” Alilalamika kada mmoja wa CCM.

Habari zaidi kutoka kwa Makada mbalimbali wa CCM zinasema kuwa uchaguzi wa Mkoa wa Magharibi unatajwa kuwa ni mfano mbaya wa ukiukwaji wa haki na taratibu za Chama hicho.

Wakati hayo yakitokea Mkoa wa Magharibi, huko Mkoa wa Kaskazini Unguja nako vituko na ukiukwaji wa taratibu umeripotiwa ambapo kura zimehesabiwa mara kadhaa zinaonesha mtu kushinda,lakini zilipohesabiwa kwa mara ya tatu anaonekana mgombea ameshindwa.

” Hapa hapakuwa na uchaguzi, ni vurugu, visa, vitimbi na ukiukwaji wa taratibu” Alisema Kada mmoja wa CCM aliyekuwa katika Uchaguzi huo.

Habari kutoka Mkoa Kaskazini Unguja zinaeleza kuwa baadhi ya watendaji wa Serikali walionekana wazi wazi kutoa maelekezo ya upendeleo kwa baadhi ya wagombea kinyume kabisa na taratibu za CCM kwani huo ni Uchaguzi ndani ya Chama na Watendaji wa Serikali hawapaswi kujishughulisha na lolote.

Kwa upande wa Mkoa wa Kusini Unguja nako hali ilikuwa kama ilivyo kwa Mikoa mengine ya Unguja, vituko vilitawala kutaka kuwabeba baadhi ya Wagombea wasiotakiwa na wajumbe.

” Hapa walilazimisha baadhi ya vigogo washinde, lakini hilo hatukukubali, tumewashinda, wakajaribu kumuongezea kura kigogo mmoja tukalibaini” Alisema Kada wa CCM Kusini Unguja.

Habari kutoka Kisiwani Pemba ambapo huko kumetajwa kukiukwa kabisa taratibu na wagombea kupendelewa wazi wazi kwa usaidizi wa Watendaji wa Serikali kinyume kabisa na Utamaduni na mazoea ndani ya CCM.

Wanachama na Makada mbali mbali waliozungumza kwa nyakati tofauti wanalalamikia vitendo vya rushwa, kubebana , maelekezo na Watandaji wa Serikali kuingilia Chaguzi hizo.

Akizungumzia malalamiko hayo, Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo amesema wanachunguza uchaguzi wa Mkoa wa Magharibi Kichama na ikibainika taratibu zilikoukwa watafuta matokeo ya Uchaguzi.

Mwisho.

Share this news

Facebook
Twitter
LinkedIn
WhatsApp

This Year’s Most Read News Stories