Tanzania: Serikali lazima ikomeshe deni la ndani

Tanzania: Serikali lazima ikomeshe deni la ndani

Dar es Salaam, Tanzania: 

Chama cha ACT Wazalendo kimeishauri Serikali kuja na mpango mkakati maalum wa kibajeti utakaosaidia kumaliza deni la ndani lilofikia asilimia 30 ambalo athari zake zitaendelea kuwaumiza wananchi.

Ripoti ya mwezi ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inaonyesha kuwa ndani ya mwaka mmoja, deni la ndani limeongezeka kwa asilimia 10 kutoka Sh18.6 trilioni hadi kufikia Sh26.6 trilioni, ongezeko ambalo alisema halijawahi kutokea kwa kipindi cha miaka 20. 

Akizungumza leo Januari 15, 2023,  waziri kivuli wa fedha na mipango wa chama hicho, Emmanuel Mvula amesema kukua kwa deni hilo kunatokana na Serikali  kukopa  zaidi  kwenye  benki za ndani, mifuko ya hifadhi ya jamiii, bima na watu binafsi kwa kuwapatia hatifungani.

“Serikali imekopa asilimia 27 ya deni la ndani na kwenye deni hilo asilimia 28 limekopwa kutoka Taasisi za fedha, asilimia 18 zinatoka bima na asilimia nyingine kwa watu binafsi.Kwa kipindi cha miaka 20 kumekuwa na ukuaji wa hili,” amesema

Amesema kukua kwa deni la taifa hasa deni la ndani, athari zake zinakwenda moja kwa moja kwa wananchi huku akieleza deni la ndani halitakiwi kuzidi asilimia 20 na kama nchi tuko asilimia 10 zaidi.

“Athari yake nyingine ifahamike tunatumia fedha nyingi kulipa deni, makusanyo yetu ya ndani yanatumika kulipa deni. Tunatumia Sh900 bilioni kwa mwezi kulipa deni la Taifa. Kila mwezi tunalipa na kati ya hizo Sh600 bilioni zinatumika kulipa deni la ndani na Sh300 bilioni zinalipa deni la nje,” amesema Mvula.
Amesema kutokana na hali hiyo serikali hiyo hutumia fedha nyingi kulipa madeni kuliko kufanya maendeleo na kwa kuwa inakopa kweye benki za ndani na kusababisha taasisi hizo kushindwa kushusha riba kwa sekta binafsi na watu wa kawaida waaohitaji mikopo.

“Ili tupate fedha za kulipa deni ndio unaona kuna utitiri wa kodi,athari nyingine tunakwenda kukopa kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii ,maana yake tunakwenda kuathiri mifuko hiyo na hivyo wastaafu kutolipwa pensheni zao.
“Madeni hayo yanasababisha mzigo mkubwa kwa wananchi. Kutokana na maelezo hayo, ACT Wazalendo tunatoa pendekezo ili kuondoa deni hili, Serikali ije na mkakati maalum wa kumaliza deni hilo kwenye bajeti ya mwaka huu na kwa kuwa tunakwenda kwenye maandalizi ya bajeti basi tunaitaka Serikali ije na mkakati wa kumaliza deni,” amesema.

Source: mwananchi.co.tz

Original Media Source

Share this news

Facebook
Twitter
LinkedIn
WhatsApp

This Year’s Most Read News Stories