Rais Mwinyi aondoa ushuru wa sukari Zanzibar

Rais Mwinyi aondoa ushuru wa sukari Zanzibar

Unguja. Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi amesema Serikali imeondoa ushuru wa Ongezeko la Thamani (VAT) kwa bidhaa ya sukari inayoingizwa Zanzibar ili kupunguza gharama za bidhaa hiyo.

Wakati Serikali ikiondoa ushuru huo wa asilimia 15, Dk Mwinyi amewataka wafanyabiashara kuacha tabia ya kuongeza bei za bidhaa linalowaumiza wananchi wasiokuwa na uwezo kumudu gharama kubwa.

Kwa sasa kilo moja ya sukari Zanzibar inauzwa kwa Sh3,200 kwa bei ya rejareja.

Dk Mwinyi ametoa kauli hiyo leo Februari 26, 2024 kwa nyakati tofauti alipofanya ziara maalumu ya kutembelea soko la bidhaa Jumbi, Darajani, Soko la samaki Malindi na Bandari ya Mizigo Malindi kuona hali halisi ya uuzaji wa bidhaa mbalimbali.

Hatua hiyo ni kuelekea kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhan  unaotarajia kuanza Machi huu.

Ametumia fursa hiyo kuwataka wafanyabiashara kuacha kupandisha bei za bidhaa makusudi kwasababu ya mfungo wa Ramadhani kwa ajili ya kujiongeza faida.

“Serikali imeshachukua jitihada za makusudi kuondoa ushuru wa VAT katika sukari inayoingizwa nchini ili kuzuia isiendelee kupanda bei wakati tunaelekea katika mwezi mtukufu wa ramadhani,” amesema Dk Mwinyi.

Amesema bei ya sukari nje ya nchi imepanda bei, ani ilikuwa ikinunuliwa tani moja kwa Dola 500 za Marekani (Sh1,150,000) na sasa Dola750 mpaka 800 (Sh1,840,000).

“Kwa hiyo tukiacha ushuru ule ule ikaja sukari humu ndani, lazima itakuwa juu lakini tulichosema kuanzia sasa mpaka bei za nje itakapokuwa sawa, tunaondoa ushuru wa VAT kwenye bei ya sukari,” amesema Rais Mwinyi.

“Ombi langu tena tusije tukaondoa ushuru halafu sukari huku ikabaki bei kubwa, mtu kama huyu tutapambana naye, maana haiwezekani huku tukupunguzie lengo liwe ni kuwasaidia watu, halafu wewe mfanyabaishara unataka kujitajirisha baada ya kuondoa ushuru.”

Amesema kufanya hivyo ni kuwaumiza wananchi wanyonge.

 “Kama leo mhogo, ndizi na nafaka zingine vinatoka hapa kwetu havina ushuru, kuna sababu gani kwa wafanyabiashara  kupandisha bei,” amehoji.

Awali, Mwenyekiti wa Wafanyabaishara wa Soko la Darajani, Muhamed suleiman amesema mfumko wa bei unawaumiza sio wafanyabaishara tu bali hata wananchi.

Akiwa sokoni hapo wajasiriamali wadogo wamemueleza kiongozi huyo jinsi wanavyosumbuliwa na kunyang’anywa mali zao na baadhi ya viongozi wakisingizia kuwa ni maagizo yao.

Zuhura Mohamed Khalfan anayejihusisha na biashara ndogo ndogo katika eneo hilo, amelalamikia kunyang’anywa bidhaa ilhali Serikali ilisema wajiajiri kwa sababu haina  uwezo wa kuajiri watu wote.

“Mheshimiwa Rais kwa kweli tunakutana na changamoto, sote tunatafuta riziki lakini tunasombewa bidhaa zetu, mimi hapa ndio mama ndio baba nina watoto sita wote wananitegemea, lakini tunapotafuta na kusombewa bidhaa zetu wanataka tuishi wapi,” amehoji.

Suleiman Mzee amesema wanakabailiwa na changamoto kubwa ya ushuru wanaposafirisha ng’ombe mmoja kutoka Tanzania bara.

Akizungumzia kero za wafanyabiashara hao, Dk Mwinyi amesema Serikali haina lengo la kumsumbua mtu na hakuna maelekezo yake aliyoyatoa kwamba wanyang’anywe bidhaa zao bali viongozi wanaotumia kauli hiyo ni dalili ya kutokujiamini katika majukumu yao.

“Kati ya vitu vinanikera sana hii kauli za kwamba tumeagizwa na Rais, hakuna Rais wa kuagiza wananchi wake wasumbuliwe, lengo Serikali inaweka mazingira mazuri ya kufanya biashara, wizara zinazohusika, viongozi wa mkoa na manispaa mjipange kuhakikisha hili halitokei tena,” amesema.

Akiwa bandari, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Bandari (ZPC), Akif Ali Khamis amemueleza Rais Mwinyi kuwa kwa siku wanapakua wastani wa makontena 200.

Amesema kwa sasa kuna kontena 114 zina bidhaa za mchele, kontena 153 za mafuta ya kula na kontena 11 za bidhaa za tende zinazosubiriwa kushushwa kwa ajili ya mwezi mtukufu.

“Kuna meli nyingine sita zinakuja zimebeba shehena ya bidhaa za vyakula, kwa jinsi vitu vinavyokuja hatutegemi kama kutakuwa na upungufu wa bidhaa,” amesema Khamis.

Amesema kwa kipindi hiki wataongeza muda wa kupakua mizigo ili kuhakikisha havikwami bandarini na wataongeza pia muda wa kufanya kazi hadi usiku ili kupunguza bidhaa kukaa bandarini muda mrefu.

“Tunachoomba wafanyabiashara wamalize taratibu zao mapema iliwatuletee taarifa tujipange biadha zitoke mapema na wananchi na watumiaji wa bidhaa wafaidike na hilo,” amesema.

Source: mwananchi.co.tz

Original Media Source

Share this news

Facebook
Twitter
LinkedIn
WhatsApp

This Year's Most Read News Stories