Siku tisa kuelekea uchaguzi, zinahitaji haya

Dar es Salaam. Wakati sekunde zikizidi kuyoyoma, saa zikikimbia na siku tisa tu zikisalia kabla ya Watanzania kuelekea kupiga kura katika uchaguzi wa serikali za mitaa, kila mmoja ana wajibu wa pekee kuhakikisha anashiriki kikamilifu kwenye mchakato huu wa kidemokrasia.

Uchaguzi huo, uliopangwa kufanyika Novemba 27, 2024 una nafasi kubwa ya kubadili mustakabali wa jamii zetu kwa miaka mitano ijayo.

Hii ni nafasi ya kuandaa daraja la maendeleo au kujiweka katika mahangaiko na changamoto za kijamii na kiuchumi.

Kwa siku tisa zilizosalia kuelekea uchaguzi huo, kuna mambo ya msingi unayopaswa kuzingatia.

Ulijiandikisha

Ni muhimu kila mpiga kura kuhakikisha majina yake yameorodheshwa kwenye daftari la wapiga wakazi.

Daftari hilo, ndilo linalotumika kuorodhesha majina ya wakazi wa maeneo husika na ndilo linalokuhalalisha kushiriki kupiga au kupigiwa kura.

Kwa mujibu wa Tume Huru ya TaiFa ya Uchaguzi (INEC) mwaka 2019, zaidi ya wapiga kura milioni sana walijiandikisha, lakini takriban asilimia 15 hawakujitokeza kupiga kura kwa sababu ya changamoto za kutothibitisha majina yao mapema.

Katika siku hizi chache, ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha hana vikwazo vya kiutaratibu na sheria vinavyomzuia kushiriki mchakato huo.

Wagombea na sera zao

Kwa siku zilizobaki Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na vyama vya siasa vina jukumu la kuhakikisha wananchi wanapata taarifa za kina kuhusu wagombea.

Kwa sababu tayari uteuzi umeshafanyika na pazia la kampeni linaenda kufunguliwa, sera ndizo zitakazoamua ushindi wa mgombea.

Uchaguzi si sherehe ya majina maarufu bali ni mchakato wa kuchagua viongozi wenye uwezo wa kuleta maendeleo.

Katika uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2019, utafiti wa Repoa ulionyesha asilimia 45 ya wapiga kura hawakujua kikamilifu sera za wagombea wao, jambo lililochangia uchaguzi wa viongozi wasiowajibika kwa jamii.

Mpiga kura anapaswa kutumia siku hizi tisa zilizobaki kuhudhuria mikutano ya kampeni, zitakapozinduliwa, kusoma ilani za vyama na hata kuuliza maswali magumu ili kufanya maamuzi sahihi.

Amani na utulivu

Historia ya Tanzania imejaa mifano ya mafanikio ya kuendesha chaguzi kwa amani.

Lakini tunapaswa kuwa waangalifu dhidi ya kauli na vitendo vinavyoweza kuchochea vurugu.

Mwaka 2020, ripoti ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), ilionyesha asilimia 20 ya vurugu za uchaguzi zilitokana na mivutano ya kidini na kikabila, hasa wakati wa kampeni.

Sasa ni wakati wa kudumisha mshikamano, kuelekeza mijadala kwenye hoja badala ya chuki na kuhakikisha tunaacha mfano bora kwa kizazi kijacho.

Hamasa kwa wapiga kura

Ushiriki wa wananchi katika uchaguzi ni ishara ya nguvu ya kidemokrasia.

Katika uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2019, ni asilimia 65 tu ya waliojiandikisha walijitokeza kupiga kura.

Takwimu hizo zinaonyesha bado kuna kazi kubwa ya kuwahamasisha watu kushiriki.

Familia, marafiki na majirani wanapaswa kushirikiana kuhamasishana ili ifikapo Novemba 27 kila mmoja awe sehemu ya mabadiliko.

Kuimarisha maandalizi ya siku ya uchaguzi

Kwa wapiga kura, kuhakikisha wanajua vituo vyao vya kupigia kura ni hatua muhimu.

Hii husaidia kuepuka msongamano na kuchanganyikiwa siku ya uchaguzi.

Kwa mujibu wa ripoti ya INEC 2019, asilimia 10 ya wapiga kura walishindwa kupiga kura kwa wakati kwa sababu ya kushindwa kufika vituoni mapema.

Kwa mamlaka zinazohusika, hatua hizi chache zilizobaki ni fursa ya kuhakikisha vifaa vyote vya uchaguzi vipo tayari, watumishi wamepewa mafunzo ya kutosha, na mazingira ya vituo vya kura ni rafiki kwa wapiga kura wote, wakiwemo wazee, wanawake wajawazito na watu wenye ulemavu.

Kujiepusha na rushwa, uvunjifu maadili

Rushwa imeendelea kuwa changamoto katika chaguzi mbalimbali.

Transparency International iliripoti mwaka 2020 kwamba asilimia 18 ya wapiga kura walirubuniwa kwa njia ya rushwa ili kuwachagua wagombea fulani.

Wakati huu tunapokaribia siku ya uchaguzi, ni muhimu kuhakikisha maamuzi ya wananchi hayashawishiwi na zawadi za muda mfupi, bali yanatokana na utashi wa kweli wa mabadiliko.

Kulinda haki za wengine

Kila mmoja ana haki ya kupiga kura kwa uhuru na usalama.

Mikutano ya kampeni inapaswa kuheshimu sheria za uchaguzi na wapiga kura wanapaswa kuacha tabia ya kuwakatisha tamaa wengine kushiriki.

Kwa mujibu wa sheria za uchaguzi nchini, vitendo vya kuwatishia wapiga kura vinaweza kusababisha kifungo cha hadi miaka mitatu jela.

Kujiandaa kisaikolojia na kifamilia

Katika siku hizi chache, ni muhimu kuhakikisha kwamba familia zimetayarishwa kwa siku ya uchaguzi.

Hakikisha watoto wapo salama, na ratiba ya siku hiyo imepangwa vizuri ili kuepusha mizozo.

Uchaguzi ni suala la kijamii linalohitaji mshikamano wa kifamilia na kijamii.

Siku tisa zinaweza kuonekana kuwa chache, lakini zinaweza kuwa msingi wa kuleta mabadiliko makubwa.

Kama Taifa, tunapaswa kutumia kila saa iliyobaki kuhakikisha tunajiandaa kwa njia sahihi kushiriki katika zoezi hili muhimu.

Huu ni wakati wa kuonyesha uzalendo kwa kuchagua viongozi wanaostahili na kuhakikisha kuwa demokrasia yetu inazidi kuimarika.

Tukumbuke kwamba kila kura ina uzito mkubwa. Kwa kila mmoja wetu anayejitokeza kupiga kura, tunaandika ukurasa mpya wa historia ya Taifa letu.

Tafakari, jipange na uhakikishe siku ya Novemba 27 inakuwa ya kipekee kwa maendeleo yetu.

Vyombo vya habari pia vina nafasi muhimu ya kuhakikisha vinaripoti taarifa bila kuegemea upande wa chama chochote cha siasa.

Kwa mujibu wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), uandishi wa uchaguzi unapaswa kuwa wa uwiano, kuzingatia maadili na kutoa fursa sawa kwa wagombea wote.

Katika siku hizi tisa, vyombo vya habari vina jukumu la kuelimisha wapiga kura, kufichua changamoto za kiutaratibu, na kupaza sauti za wananchi wanaotafuta mabadiliko.

Huu ni wakati wa kuonyesha uzalendo kwa kuchagua viongozi wanaostahili na kuhakikisha kuwa demokrasia yetu inazidi kuimarika.

Tukumbuke kila kura ina uzito mkubwa. Kwa kila mmoja anayejitokeza kupiga kura, anaandika ukurasa mpya wa historia ya Taifa.Continue Reading

Kona ya Maloto: Barabara za Dar ni hatari zaidi kwa vyombo vya moto

Dar es Salaam, lango kuu la kiuchumi Tanzania, barabara zake ni hatari kwa magari. Barabara kuu zote zipo kwenye ujenzi, zile za mitaani na zenye kuunganisha vitongoji, zimesheheni mashimo.

Hatari zaidi, upo mfumo wa kuziba mashimo kwa kuweka viraka. Mafundi wanachonga lile shimo, wanalitanua na kulipa umbo la pembe nne. Baada ya utanuzi huo, wanaliacha hadi miezi miwili. Hatari kwa madereva, hasa wageni wa barabara husika.

Wazoefu huendesha kwa uzoefu. Anafika mahali anapunguza mwendo kwa sababu ameshajua shimo lililochongwa lipo karibu. Hakuna taa wala alama za tahadhari kuwa mbele kuna shimo.

Miezi michache iliyopita nchi ilipita kwenye mafuriko. Dar es Salaam iliathirika. Miundombinu ikatoneshwa, sasa ni mibovu ajabu. Zile hadithi kuwa watu wanaoishi mabondeni ndiyo hawapo salama, tafsiri inahama.

Dar es Salaam kila sehemu ni bondeni. Hata maeneo yaliyopo uwanda wa juu yalikumbwa na mafuriko na sasa barabara ni taabani. Unapoendesha gari Dar es Salaam, nenda taratibu. Utaua chombo, unaweza kupoteza maisha pia.

Anzia Mikocheni hadi Tegeta, Mbezi Beach mpaka Ununio, usiku unaweza kukuta magari mitaroni. Ukimuuliza dereva, anasema alikuwa anakwepa shimo. Mwenyewe aliendesha mwendo wa kasi akidhani barabara ni salama. Dar siyo salama.

Ujenzi holela, fedha zinazidi nguvu sayansi. Utatuzi wa matatizo kwa kutumia mawazo kidogo yenye mtazamo wa muda mfupi, badala ya kufikiria miaka mingi ijayo. Hapa ndipo nchi inaumizwa na inauawa taratibu. Bila hatua za haraka tutarithisha watoto na wajukuu nchi mfu.

Mvua kidogo, barabara zinatengeneza matundu kila mahali. Dar es Salaam haina barabara ambayo unaweza kuendesha japo kilomita 120 kwa saa, hata kama barabarani upo peke yako na hakuna alama za udhibiti mwendo. Sababu barabara ni mbovu, haziaminiki. Ni mitego tupu kwa madereva.

Barabara zinazojengwa, zinabanwa na kuwekewa matofali yenye kuakisi taa. Yale matofali barabarani ni salama kama dereva unaendesha kipindi ambacho hakuna gari lingine linatokea unapoelekea. Hatari zaidi, dereva wa gari linalokuelekea awashe taa kali. Hutaona tofali. Madereva wengi huyagonga matofali na kuharibu magari.

Askari wa usalama barabarani na magari ya breakdown, kwao ni mtaji gari likigonga tofali barabarani. Mimi ni shuhuda wa tukio la gari aina ya Toyota IST, liligonga tofali eneo la Makumbusho, Kijitonyama, mbele ya Millenium Tower. Kulitoa gari pale kulipeleka Kituo cha Polisi Kijitonyama, kadirio la kilomita moja na nusu, breakdown walilipwa Sh250,000 na trafiki akataka apewe Sh150,000, eti ili amalize kesi.

Trafiki akasema, asingelipwa hiyo pesa, angeandika ripoti kwenda Tanroads kuwa gari lile, IST, liliharibu tofali la ukingo wa barabara. Ukiangalia, tofali ni zima, IST uso wa mbele umeharibika, hadi mifuko ya usalama (airbags), ilitoka.

Ni Tanzania na Watanzania. Trafiki (askari wa usalama barabarani), anafika kwenye ajali, hataki kujua watu ndani ya gari wapo salama kiasi gani, anaomba Sh150,000, eti ndiyo amsaidie mwenye gari kuepuka kesi. Unajiuliza, hata ukienda mahakamani, kesi ya uzito gani?

Kuhusu ubovu wa barabara Dar es Salaam, mashimo na uwekaji viraka unaochukua muda mrefu, inadhihirisha namna ambavyo ujenzi unafanyika chini kabisa ya viwango mbele ya viongozi wanaoomba bajeti, wanaopewa na kuzisimamia. Wataalamu pia wapo.

Janga la taifa ni rushwa na ufisadi. Viongozi na wataalamu wanaotegemewa kuisaidia nchi, wanafuja fedha za miradi, matokeo yake miundombinu inajengwa nchini ya kiwango. Makandarasi wanahonga kushinda zabuni. Vigezo vya kisayansi havina tija mbele ya mlungula.

Kifo cha nchi ni kuwa na viongozi wenye kuwaza leo badala ya kesho. Matatizo mengi Dar es Salaam ni ujenzi unaoingilia njia za maji. Mwenye fedha anahamisha uelekeo wa maji, matokeo yake madhara makubwa hutokea pale mvua zinaponyesha mfululizo. Maji yanapanda hadi kwenye miinuko.

Kama mapinduzi ya fikra hayatakaribishwa Tanzania, ikapatikana tiba ya jinsi ya kutatua matatizo ya watu kwa usahihi, rushwa ikachukiwa kutoka ndani ya fikra na moyoni, suluhu zikatazamwa za kudumu na kujenga dhamira ya kuiacha nchi salama kwa vizazi vijavyo, historia itatoa hukumu mbaya kwa hiki kizazi chetu kinachoishi sasa.

Ukipita Unguja, kasi ya ujenzi wa barabara ni kubwa. Barabara bora na imara kabisa. Unaweza kupata jawabu kwamba miaka mitatu ijayo, Unguja (Zanzibar), itakuwa jiji lenye barabara nzuri na za uhakika, wakati Dar es Salaam ikibaki hohehahe na barabara zake zinazoua magari.Continue Reading