Ndoa za utotoni kichocheo cha ukatili kijinsia

Dar es Salaam. Wakati Tanzania ikiungana na mataifa mengine duniani katika kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, moja ya vitu vinavyotajwa kuchochea ukatili huo ni ndoa za utotoni.

Miongoni mwa changamoto zinazotokana na ndoa za utotoni ni unyanyasaji wa kimwili, ikizingatiwa wanaoolewa kuna nyakati hukumbana na vipigo na mateso kutoka kwa wenza wao na hata ndugu, hivyo kukiuka haki zao za msingi.

Si hayo pekee, ndoa hizi husababisha ukatili wa kijinsia wa kihisia na kisaikolojia. Watoto wanaolazimishwa kuingia kwenye ndoa mara nyingi wanakosa uwezo wa kujieleza, kushiriki maamuzi ya familia, au kudai haki zao. Wanapozuiliwa kujieleza, wanapewa jukumu la kuwatunza watoto au familia wakiwa bado hawajakomaa, jambo linalowaathiri kisaikolojia.

Pia husababisha unyanyasaji wa kiuchumi, watoto hukosa fursa ya kupata elimu na kushiriki katika shughuli za kiuchumi.

Kukosa elimu na fursa za kiuchumi kunawaweka katika hali ya utegemezi wa kifedha kwa waume zao, hivyo kusababisha hatari ya kunyanyaswa kijinsia kwa kutokuwa na uwezo wa kujitegemea.

Ni kutokana na ndoa hizi, watoto huathiriwa kwa kuzaa mapema kabla miili yao haijakomaa, hali ambayo huongeza hatari ya matatizo ya kiafya kama vile fistula, kifafa cha mimba na hata vifo vya uzazi.

Ndoa za utotoni huwanyima wasichana nafasi ya kujenga mahusiano yenye usawa, badala yake, wanajikuta wakitumikishwa nyumbani, na kubaguliwa.

Kwa mujibu wa Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya

Malaria Tanzania (TDHS-MIS) mwaka 2022, asilimia 20.3 ya Watanzania wenye miaka 15-19 wameolewa, wanaishi pamoja au walikwisha kuwa kwenye mahusiano na wametengana. Kati ya walioolewa wa umri huo asilimia 30.6 wanandoa zilizosajiliwa na wana vyeti.

Vilevile takwimu hizo zinaonyesha wanawake wenye miaka 25-49 waliolewa wakiwa na wastani wa miaka 19.8.

Utafiti unaeleza elimu na hali ya umasikini vinachangia kwa kiwango kikubwa, kwani wastani wa umri wa wanawake wasio na elimu na ni masikini kuolewa ni miaka 18.1 ukilinganisha na wale waliohitimu sekondari au elimu ya juu walioolewa na miaka 23.7.

Hata hivyo, takwimu zinaonyesha wanawake huanza kujihusisha na ngono miaka mitatu kabla ya kuolewa wakiwa na wastani wa miaka 17 na wanaolewa wakiwa na miaka 19.8.

Baadhi ya viongozi wa dini wamekuwa na maoni mbalimbali yanayopingana na ndoa za utotoni.

Padri Longino Rutangwelera anasema Kanisa Katoliki haliungi mkono ndoa hizo, akieleza maana ya ndoa katika mustakabali wa dini.

Padri Rutangwelera anasema katika dini ndoa ni maagano ya watu wawili waliokomaa kimwili na kiakili na si vinginevyo.

“Ndoa ina wajibu wake, misingi na haki zake inamtaka mtu awe na ukomavu wa kiakili na kiimani pia, unapomlazimisha msichana kuingia kwenye ndoa za utotoni unapingana na uhalisia,” anasema.

“Kumuoza binti ambaye hajakomaa kiakili, kimwili na kifikra ni kupingana na matakwa na mapenzi ya Mungu na kupingana na uhalisia.

“Unapomlazimisha mtoto kuingia katika ndoa anakosa elimu na kuingizwa kwenye makubaliano ambayo kwa akili na ukomavu wake hana uelewa wa kutosha, hivyo atapata watoto wakati uwezo wake wa kuwa mama au baba hautoshi, ni vema wakaachwa hadi wawe wakomavu, kimwili, kiakili na kihisia ili kupokea majukumu hayo kikamilifu,” anasema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), Sheikh Khamis Mataka anasema kuna umuhimu wa kutenda uadilifu kwa kuwapa nafasi sawa watoto wa kiume na wa kike, ikiwamo suala zima la kupata elimu kwa kadri ya uwezo wao.

“Hata hivyo, bado kuna changamoto kwa mtoto wa kike, ikiwamo ya kuozwa katika umri mdogo na kukosa haki yake ya kielimu.

“Ninachokitamani ili kuondoa ukatili huu, kuwepo sheria ambayo itamsaidia mtoto wa kike kutoingia kwenye ndoa za utotoni,” anasema.

Akifafanua kuhusu Sera ya Elimu ya mwaka 2014, Sheikh Mataka anasema imeweka kidato cha nne kuwa ni elimu ya lazima.

Kiongozi huyo anasema kama sera itaongezwa na kudadavua kwamba elimu ya lazima iwe kidato cha sita, itamsadia mtoto wa kike.

“Hadi atakapohitimu kidato cha sita, huyu mtoto atakuwa amefikisha miaka 17 hadi 18, katika umri huu changamoto cha ndoa za utotoni itakuwa imeondoka,” anasema.

Anasema Sheria ya Ndoa namba 5 ya mwaka 1971 nayo itamke mwanafunzi wa elimu ya lazima haruhusiwi kuoa wala kuolewa na Sheria ya Elimu namba 5 ya mwaka 1978 iseme mtoto haruhusiwi kuoa wala kuolewa hadi ahitimu elimu ya lazima, hivyo itasaidia kuwalinda watoto wa kike.

“Atakapohitimu elimu ya lazima atakuwa amepata ukomavu ambao hata akiolewa atakuwa na uwezo wa kulea familia,” anasema.

Mchugaji Monica Lugome wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mashariki na Pwani anasema ajenda kubwa ya kumlinda mtoto wa kike na ndoa za utotoni ni kutoruhusu aolewe chini ya miaka 18.

Anasema anapoolewa chini ya umri huo ni mateso kwake na hata vitabu vya dini haviruhusu hilo.

“Biblia inatuagiza kumlea mtoto katika njia impasayo ikiwamo kuhakikisha anapata haki zake katika nyanja zote ikiwamo elimu. Unapomuoza katika umri mdogo ni kumnyima haki yake ya msingi,” anasema Mchungaji Monica.

Mjadala wa kitaifa

Taasisi ya kimataifa ya Norwegian Church Aid iliandaa mjadala wa kitaifa kujadili umri sahihi wa kuoa au kuolewa, uliowahusisha wadau mbalimbali kutoka mikoa 10 nchini.

Msimamizi wa miradi wa taasisi hiyo Tanzania, Sarah Shija anasema mjadala huo uliofanyika Novemba 28, ulilenga kukosoa na kushauri kuhusu changamoto zinazosababisha ukatili wa kijinsia.

“Hii itasaidia kuleta mabadiliko, kuna makundi kama viongozi wa dini yana nafasi na ushawishi katika mabadiliko ya kisheria, hususani kwenye umri wa binti kuolewa na madhara ya ndoa katika umri mdogo,” anasema.

Rebeca Gyumi, Mkurugenzi wa Taasisi ya Msichana Initiative anasema pamoja na mambo mengine, mjadala huo pia umeangalia uzoefu wa nchi mbalimbali kwenye masuala ya mabadiliko ya umri wa ndoa.

Rebeca aliyefungua kesi za kikatiba kupinga vifungu vya 13 na 17 vya Sheria ya Ndoa vilivyotoa mwanya kwa watoto wa kike kuolewa wakiwa na umri wa miaka 14 kwa kibali cha Mahakama na umri wa miaka 15 kwa ridhaa ya wazazi, anasema mchango wa viongozi wa dini ni mkubwa ili kufikia lengo la kutokomeza ukatili wa kijinsia, hususani ndoa za utotoni.

Rachel Boma, kutoka Shirika la UN Woman Tanzania anasema nchi mbalimbali zimefanya mabadiliko ya kisheria na kuweka umri wa ndoa kuwa miaka 18.

“Nchi kama Indonesia au Misri ambazo mfumo wao wa sheria ni kama kwetu, Serikali ziliona mabadiliko katika sheria zao na wao umri wa kuolewa ni miaka 18, hivyo katika mijadala kama hii tuna vitu vingi vya kujifunza kutoka kwa wenzetu.

Akizindua kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi, alisema Serikali itayajadili maombi yote yaliyotolewa na mtandao wa kupinga ukatili wa kijinsia (Mkuki) ikiwamo suala la kutunga sheria mahususi ili kushughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia na kuyatokomeza.

Alisema watakaa pamoja kuyajadili ili kuona namna gani hatua mbalimbali zinaweza kuchukuliwa.

”Katika sheria zetu mbalimbali tuna sheria nyingi zinazopinga ukatili wa kijinsia na zinaelezea masuala hayo na kutoa adhabu kali ikiwemo Sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 mkiisoma sheria hiyo imeelezea ukatili katika maeneo mengi,” alisema.

Kampeni hiyo iliyozinduliwa Novemba 23 itafikia tamati Desemba 10. Kaulimbiu ni ‘Kuelekea miaka 30+ ya Beijing, Chagua kutokomeza ukatili.’

Kaulimbiu hiyo inawakumbusha watu kujitafakari na kitathmini yale yanayofanywa kama yana tija.

Mwenyekiti wa Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF), Dk Monica Muhoja anasema kuna haja ya kutungwa sheria maalumu kupinga ukatili wa kijinsia.

“Mwaka huu tumekuja na maombi mengine ikiwamo kufika kwenye ajenda za kiusalama kuhakikisha masuala ya ukatili wa kijinsia yanaingizwa rasmi katika mipango na mikakati ya kiusalama ya kitaifa,” alisema.

Mkurugenzi wa WiLDAF, Anna Kulaya alisema dhamira ya kampeni hiyo ni kushawishi na kuhamasisha jamii kuondoa mitazamo inayochochea unyanyasaji na ukandamizaji wa kijinsia huku ikikuza usawa, heshima na haki kwa wote.Continue Reading

Waziri Mkuu kuongoza matembezi ya kusaidia wenye ualbino

Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ataongoza matembezi ya hisani kwa ajili ya kuelimisha jamii kuhusu watu wenye ualbino.

Matembezi hayo yaliyoandaliwa na Taasisi ya Lions Club ya Dar es Salaam, Tanzanite na Sky kwa kushirikiana na Chama cha wenye ualbino Tanzania (TAS), yatakwenda sanjari na uchangiaji wa fedha kwa ajili ya kusaidia mahitaji ya kibinadamu kwa kundi hilo.

Akizungumzia matembezi hayo yaliyopewa jina la Sunset Charity Walk, Kaimu Mwenyekiti wa TAS, Abdillah Omar amesema watu 1,000 wanatarajiwa kushiriki kwenye matembezi hayo.

Matembezi hayo ya kilomita tano yatafanyika kesho, Jumamosi ya Novemba 30, 2024 saa 11 jioni, kuanzia Ocean Road kwenda hadi daraja la Tanzanite.

“Tunaamini watu wengi watajitokeza kuungana nasi kutuunga mkono katika matembezi haya ambayo tunayafanya kwa mara ya kwanza kwa kushirikiana na Lions Club,” amesema.

Gavana wa Lions Club Tanzania, Habil Khanbhai amesema hii itakuwa mara ya kwanza kwa taasisi hiyo kusaidia watu wenye ualbino na wanatarajia kuendelea kushirikiana nao na kuwaunga mkono.

Mbali na elimu itakayotolewa kwa jamii ili ipate uelewa kuhusu watu wenye ualbino, pia matembezi hayo yanalenga kukusanya fedha kwa ajili ya kusaidia mahitaji mbalimbali ya kibinadamu kwa kundi hilo.

“Tunatarajia kuwa na watu 300 wenye ualbino, watu 100 kutoka Jeshi la Polisi na watu wengine kutoka maeneo mbalimbali,” amesema Khanbhai akisisitiza jamii kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuliunga mkono kundi hilo sambamba na kujisajili kwa gharama ya Sh20,000.

Mkuu wa Utafiti wa Jeshi la Polisi, SACP Ralph Meela amesema jeshi hilo limekuwa likishirikiana kwa karibu na kundi hilo ikiwamo kuzielimisha jamii ambazo zimekuwa na imani potofu kuhusu ualbino.

“Kwa muda mrefu tumekuwa tukifanya hivi na hata matukio ya kikatili dhidi ya ndugu zetu hawa (wenye ualbino) yalitulia na tangu 2022 tulikuwa tumeyasahau, hivi karibuni ni kama yameibuka , tunaendelea kuyatokomeza,” amesema.Continue Reading

Wajawazito Uzi, Ng’ambwa wanavyosotea huduma

Unguja. Licha ya kuwa na kituo cha afya kilichojengwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf), wajawazito wa visiwa vya Uzi na Ng’ambwa Mkoa wa Kusini Unguja, wanaendelea kusotea huduma za uzazi kutokana na ukosefu wa madaktari na wauguzi kwa takribani mwaka mmoja sasa.

Ng’ambwa ina wakazi 1,158 kati ya hao wanawake ni 571 na wanaume 587, huku Uzi ikiwa na wakazi 3,075 kati ya hao wanawake ni 1,510 na wanaume 1,565. Wote wanategemea kituo hicho cha afya kilichopo Kisiwa cha Uzi kwa ajili ya huduma.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Ahmed Suleiman Abdulla aliahidi siku ya ufunguzi wa kituo hicho wakati wa shamrashamra za Mapinduzi Desemba 27, 2023 kuwa kitapelekewa wataalamu wa afya.

Daktari dhamana (mganga mfawidhi) wa kituo hicho cha afya, Saleh Lilah Ali akizungumza na Mwananchi Novemba 25, 2024 ameeleza ugumu wanaokumbana nao katika utoaji huduma, akikiri kuwapo uchache wa wafanyakazi kwamba kuna muuguzi mmoja na daktari mmoja ambaye ni yeye.

Daktari huyo pamoja na muuguzi hawaishi kwenye visiwa hivyo, bali huenda kutoa huduma na kuondoka.

“Changamoto ni nyingi tunajua wanawake wapo na wanajifungua nyumbani, hawezi kuja hapa kwa sababu ya uchache wa wafanyakazi na hatuwezi kutoa huduma saa 24 kwa sababu ya uchache huohuo,” amesema Dk Saleh akiiomba Serikali iongeze wafanyakazi.

Amesema kwa mwezi mmoja wanafikisha wastani watu 300 hadi 500 wanaopatiwa huduma katika kituo hicho.

Kwa upande wa watoto, amesema wanafika takribani 100, huku wajawazito wanaohudumiwa wakikadiriwa kufikia 60 kwa mwezi.

Ili kutoa huduma nzuri kulingana na wananchi wanaohitaji huduma katika kituo hicho, Dk Saleh amesema angalau kwa uchache wanahitajika wauguzi watano na madaktari watatu.

Kwa mujibu wa miongozo ya Shirika la Afya Dunia (WHO), muuguzi mmoja anatakiwa ahudumie wajawazito wasiozidi watano.

Dk Saleh amesema wanawaelekeza wajawazito wanaofika wakati wa kujifungua, waondoke kisiwani humo kutafuta sehemu ya kuishi karibu na hospitali ambako watapata huduma zote kwa usalama.

Walichosema wanawake

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wanawake wakazi wa visiwa hivyo wamesema wanapata huduma za kujifungua Kitogani au Unguja Ukuu lakini wanakumbana na kikwazo cha barabara kwani kuna daraja ambalo halipitiki muda wote kutokana na maji kujaa na kuondoka kulingana na mfumo wa bahari.

Asha Said Ali, mkazi wa Uzi amesema: “Tunapata matatizo kila kukicha, mwanangu hivi majuzi alikuwa mjamzito, alipata uchungu nikaja naye hapa nikaambiwa niondoke naye twende Unguja Ukuu, nilipofika huko nikaambiwa nimpeleke Kitogani.

“Hapo nilisikia akili yangu kuchanganyikiwa, na uchungu tunaujua sote kina mama jinsi unavyouma, inakuwa tafrani tupu,” amesema.

Ashura Said, amesema: “Kutokana na hali hii, nimeshawazalisha wanawake watano wakiwa nyumbani kwa nyakati tofauti, hiyo ni hatari lakini ndiyo hivyo tunamuomba Mungu. Utafanyaje, inabidi ufanye hivyo kwa kubahatisha tukizidi kumuomba Mungu alete usalama.”

“Nimewahi kumzalisha mama mmoja kwenye gari wakati tunampeleka Unguja Ukuu, tulipofika kwenye daraja tukakuta maji yameshajaa, hatukuwahi kuvuka, kwa hiyo akajifungua kwenye gari lakini tunashukuru Mungu alijifungua salama,” amesema.

Hajiram Ramadhan Aidar, amesema kujifungulia nyumbani unapoteza damu nyingi na kuongeza: “Sasa hapo kuna mawili, kupoteza maisha au kunusurika.”

Mwinzuma Arah Khamis kutoka Shehia ya Ng’ambwa, naye amesema ameshawahi kuwasaidia wajawazito kujifungua.

“Kwa sisi wanawake wa huku ni changamoto kubwa, ukifika wakati wa kujifungua unaambiwa nenda mjini ili siku ya kujifungua uwe salama, lakini kama una watoto wengine roho yako inakuwa ngumu kukaa huko huku nyumbani hujui watoto wako wanaishije. Ndiyo maana unabahatisha unasubiri uchungu uje ndipo uondoke au wakati mwingine watu wanaamua kuzalia nyumbani,” amesema.

Wanaeleza kutokana na vipato vyao, wanapata changamoto kugharimia nauli za kufuata huduma ng’ambo.

“Ukichukua bodaboda, watu wawili mnalipa Sh8, 000 kama ni boti mnalipa Sh10, 000, lakini mjamzito kumpandisha kwenye pikipiki na njia yenyewe ilivyo mbovu unamwongezea uchungu mara mbili,” amesema Mwinzuma.

Mashavu Mabrouk Khamis, amesema kwa kuwa kuna tatizo la uhaba wa madaktari na wauguzi, Serikali iwaruhusu wakunga wazalishe lakini iwapatie mafunzo angalau ya miezi mitatu ili wapate ujuzi.

Amesema wakati wa kufungua kituo hicho waliahidiwa kupewa wataalamu wote lakini wanasikitika kuona ahadi haijatekelezwa.

Maliki Mbaraka Makame, amesema wataalamu wawili waliopo hawaishi katika kisiwa hicho bali hufika na kuondoka ilhali kuna nyumba kwa ajili yao.

“Sijaona mpaka sasa madaktari wakikaa hapa, wanakuja na kuondoka hatujui kwa nini inakuwa hivyo. Serikali inatakiwa iwaajiri wazawa wa hapa kijijini, hili litapunguza adha hii ya wataalamu kutokaa hapa,” amesema.

Ahmed Ali Mussa, mkazi wa Shehia ya Ng’ambwa amesema baadhi ya wanawake hawana ndugu nje ya kisiwa hicho, hivyo hushindwa kuondoka wakati wa kujifungua.

Shekha wa Shehia ya Uzi, Othman Mwinyi Haji amesema changamoto hiyo imekuwa ya muda mrefu licha ya kujengewa kituo hicho kipya bado kilio ni kilekile.

Amesema tangu kituo hicho kifunguliwe mpaka sasa ni mwaka mmoja lakini huduma zinazorota wakati mwingine wataalamu hao wanashindwa kufika kwa sababu ya maji kujaa kwenye daraja.

“Akikuta maji yamejaa anasubiri mpaka yatoke, kama yamejaa saa mbili asubuhi basi mpaka yatoke inakuwa saa nane mchana, kwa hiyo hawezi tena kuja, huku kwanza hata muda wenyewe wa kufunga kituo unakuwa umeshafika,” amesema.

Othman amesema: “Hivi karibuni mjamzito alijifungua akiwa kwenye fiber (boti) anapelekwa Unguja Ukuu, hata yule nahodha alipoona mwanamke huyo kazidiwa akaanza kujifungua, alichumpa (kuruka) ili kuwaachia wanawake wamshughulikie.”

Ameiomba Serikali iwapatie wauguzi na madaktari ambao watahudumia wananchi kwa saa 24, akieleza kituo hicho pamoja na changamoto zilizopo kinafungwa saa 9.00 alasiri.

Amesema suala la wajawazito kulazimika kwenda kwa ndugu wanapofika hatua ya kujifungua inawapa kero.

“Kuna ndugu hawapendi kukaa na watu ila mtu anamkubalia kwa sababu ya muhali tu ila kiuhalisia inakosesha amani,” amesema.

Amesema iwapo kungekuwa na njia nzuri ingewasaidia hata inapotokea dharura kuwahi kwenda ngambo katika vituo vya afya vingine.

DMO aeleza

Akizungumzia hali hiyo, Daktari Dhamana (Mganga Mkuu) wa Wilaya ya Kati Unguja, Dk Amina Hussein Pandu amesema Serikali inajipanga kuwezesha ktuo hicho kutoa huduma.

“Kitu kimoja kikubwa cha kufanya ni kuwa na gari na boti ya dharura na itafutiwe sehemu ya kukaa, hivyo ndiyo vitu wizara inajipanga navyo,” amesema.

Amesema vituo vina madaraja na hicho bado kipo katika daraja la kwanza ila kikifika la pili kitaweza kutoa huduma zote.

“Serikali inajipanga, tunaomba wawe wastahimilivu waipe muda, bado inaweka mazingira kwa kina mama. Kwa sasa kinachotakiwa angalau kuwa na boti na gari la dharura ili mama akipata uzazi pingamizi aweze kusafirishwa,” amesema.

Dk Amina amesema kituo hicho hakina uhaba wa watumishi kwa kuwa wameshapelekwa. Hata hivyo, hakuwa na jibu la moja kwa moja la idadi ya waliopelekwa na jumla ya wataalamu waliopo katika kituo hicho kwa sasa.

Kuhusu wataalamu hao kukaa kisiwani humo, amesema hawana amri ya kumlazimisha kukaa kwenye nyumba hizo kwa sababu wengine wanafamilia zao nje ya Uzi.

Kuhusu wakunga kuruhusiwa kuzalisha, Dk Amina amesema: “Wakunga wa wajadi kwa sasa tunawaomba wawapeleke wajawazito kituo cha afya ili kuepusha madhara yanayoweza kutokea.”

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Dk Khalid Mohamed Salum amesema tayari Serikali ipo kwenye mchakato wa kuweka miundombinu ya barabara na ujenzi wa daraja katika eneo hilo.

Barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 8.72 na daraja likiwa na urefu wa kilomita mbili na upana wa mita 6.5 litaweza kupitisha magari mawili kwa pamoja.

Pia kutakuwa na njia ya waenda kwa miguu na reli za kuzuia ajali. Daraja hilo amesema litakuwa na urefu wa mita nne na nusu kwenda juu.

Amesema Sh35 bilioni zitatumika katika ujenzi wa barabara na daraja hilo, hivyo kuondoa changamoto hiyo ya muda mrefu.Continue Reading

Wakopaji wanaodhalilishwa mitandaoni wapewa mbinu

Dodoma. Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC) imewataka watu wanaomba mikopo kidijitali, kusoma maelekezo vizuri ili kuepuka kuruhusu kampuni hizo kuingia katika orodha ya namba za simu (phone book) na kuwadhalilisha.

Kauli hiyo imekuja wakati baadhi ya kampuni zinazotoa mikopo kwa njia ya kidijitali, kutuma ujumbe mfupi wa maneno unaodhalilisha na wakati mwingine kutuma picha za vitambulisho vya wanaowadai.

Hatua hiyo imekuwa ikiibua malalamiko kwa jamii na hadi imekuibuliwa bungeni ambapo Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson alionyesha kukerwa na udhalilishaji unaofanywa kwa kuwashirikisha wasiohusika na mikopo hiyo.

Spika Tulia alieleza hayo Juni 27, 2024, bungeni wakati wa kipindi cha maswali na majibu akiitaka Serikali ieleze suala hilo ambalo lilikuwa likijadiliwa zaidi nje ya Bunge, “sijui kama kuna mwongozo wowote na Serikali mnalipokea na mnalifanyia kazi, hilo limekuaje.”

Aliyekuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye alijibu suala hilo akikiri kuwepo kwa changamoto hiyo ya watu ambao wanakopeshana mitandaoni na baadaye wanatuma taarifa kwa watu wanaomzunguka mkopaji.

Nape alisema Serikali imeiagiza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na Kitengo cha Kudhibiti Wizi Mtandaoni na Jeshi la Polisi kulifanyia kazi.

Aprili 1, 2024 Mwananchi iliripoti malalamiko ya baadhi ya watu wanaotumiwa ujumbe wa kuwataka kuwakumbusha waliokopa kulipa madeni yao, na jinsi kampuni zinavyopata namba hizo za simu.

“Ndugu wa karibu/jamaa/rafiki/jirani wa (jina la mkopaji na namba ya simu) aliyechukua mkopo kwa nia ya mtandao kupitia application ya… unafahamishwa kuwa mtu huyu amekiuka makubaliano kwa kutolipa deni siku husika ya marejesho na kutopokea simu za ofisi, hivyo tutamchukulia hatua kwa kosa hilo.

“Unaombwa kumpigia simu muhusika na kumjulisha kuwa ana masaa mawili ya kulipa deni kabla ya hatua kali hazijachukuliwa dhidi yake. Fanya hivyo kuepuka usumbufu.”

Leo Jumatatu, Novemba 25, 2024, Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dk Emmanuel Mkilia akizungumzia maandalizi ya warsha ya kuongeza uelewa kuhusu dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi jijini Dodoma amegusia suala hilo la udhalilishaji.

“Kimsingi tumeona kuna uvunjifu mkubwa wa sheria ya ulinzi wa Taifa, hasa watu wanaotumia mitandao wanapata nafasi kutumia picha na vitambulisho vya watu na wanatumia sms (ujumbe mfupi wa maneno) kwa watu wote walioko ndani ya simu husika hilo ni kosa kisheria,” amesema.

Amesema suala hilo wamekuwa wakilishughulikia kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kuhakikisha taasisi ndogo za fedha ziwe zimesajiliwa kisheria na BoT.

Amesema wanaofanya biashara hiyo wanatakiwa kuzingatia sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi na ndio maana wengi wamefungiwa hivi karibuni kujishughulisha na biashara hiyo.

Amesema mwananchi anapoomba mkopo kupitia programu tumizi ‘application’ hizo kwa kujua ama kwa kutokujua inakuwa ni sharti kama hutalipa deni hilo ambalo wanawataka aruhusu ili waweze kuingia kwenye orodha ya namba za simu (phone book) na kuangalia anwani ya watu unaowasiliana nao.

Dk Mkilia amesema bila kujua mwananchi anapoweka alama ya tiki, application hiyo inakuwa na ruhusa ya kuingia katika orodha ya namba za simu, hivyo hata wakati mwingine kabla ya muda wa kulipa kufika taarifa zinapelekwa za kumkashifu huyo mtu kwa watu wote anawasiliana nao.

“Kuwaasa wananchi kupitia vizuri maelekezo yanayoelekezwa mle ile usijikute kuwa ni mwathirika,” amesema.

Tayari BoT imezifungia kutoa mikopo programu tumizi (application) 69 baada ya kuzibaini zinaendesha shughuli hiyo kidijitali bila kuwa na leseni wala idhini.

BoT ilitangaza uamuzi huo Novemba 21, 2024 kupitia taarifa iliyosainiwa na Gavana wa Bot, Emmanuel Tutuba ikiutahadharisha umma wa Watanzania kutojihusisha na majukwaa na programu tumizi zilizofungiwa.

Kuhusu warsha ya kuongeza uelewa juu ya dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi, Dk Mkilia amesema warsha hiyo itafanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Desemba 17 hadi 18, 2024 ambapo washiriki ni maofisa ulinzi wa taarifa binafsi (DPOs) wa taasisi za umma na binafsi.

Amesema lengo ni kuelimisha wadau wa ulinzi wa taarifa binafsi nchini na kutoa elimu pamoja na maarifa muhimu kwa taasisi za umma na binafsi kuhusu utekelezaji wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ya mwaka 2022 na kanuni zake.

Dk Mkilia amesema katika kutekeleza agizo la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa Aprili 3,2024 wakati akizindua tume hiyo taasisi 700 za umma na binafsi zimejisajili katika tume hiyo.

Mwakilishi wa Kampuni ya Hilton Law Group ambao wanashirikiana na PDPC katika warsha hiyo, Wakili Dorothy Ndazi amesema ni muhimu kwa taasisi zote kuelewa wajibu wao kuhusu dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi.Continue Reading

Zanzibar ilivyojizatiti kuondoa urasimu bandarini

Unguja. Ukizinduliwa mpango wa maboresho ya huduma za bandari, Rais wa Zanzibar , Dk Hussein Mwinyi amesema utaleta mageuzi ya kiutendaji na kuondoa urasimu kwa kupeana majukumu kwa kila anayehusika kupitia viashiria vilivyowekwa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo uliondaliwa na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi kwa kushirikiana na Taasisi ya Tony Blair (TBI) leo Novemba 22, 2024 Ikulu Zanzibar, Rais Mwinyi amezitaka taasisi hizo kuwa tayari kuutekeleza ili ulete tija.

Mpango huo pia unazihusisha wizara tatu za Ujenzi, Biashara na Fedha na taasisi 16.

Dk Mwinyi amesema: “Iwapo kuna mmoja katika mnyororo huo hatimizi wajibu wake, atafanya kazi nzima isiende inavyotakiwa, na itabidi wafanye tathimini kila wakati kupitia viashiria vilivyowekwa na wale ambao watashindwa kutekeleza hilo nitapenda kupata taarifa ili tuchukue hatua stahiki.”

“Endapo taasisi zote zitafanya kama inavyotakiwa hakika tutapata mafanikio makubwa katika nchi yetu, hivi sasa nchi kama za Singapore, Gambia na Kenya wanatumia mfumo huo wa ushirikishwaji na wameweza kupata mafanikio makubwa,” amesema Dk Mwinyi.

Ametaja malengo mengine ya mpango huo ni kurahisiha ushushaji wa makasha, kupunguza muda wa meli kukaa ukutani na kupunguza muda wa meli kukaa nangani, hivyo kupunguza muda wa kutoa mizigo bandarini na kuongeza ukuaji wa uchumi.

Dk Mwinyi amesema Serikali imedhamiria kuendesha huduma za bandari kwa ufanisi zaidi kwa kuzingatia bandari ni mlango mkuu wa uchumi wa nchi.

Amesema mikakati ya Serikali ya ukuzaji uchumi Zanzibar inaendelea kuwawekea wafanyabiashara mazingira mazuri na sasa inatarajia kuanza ujenzi wa bandari jumuishi ya Mangapwani.

“Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote kuendeleza sekta ya bandari nchini na miongoni mwa mipango ni kuimarisha bandari za Malindi, Shumba, Mkoani, Pemba,” amesema.

Amewataa wadau wote zikiwemo kampuni za uendeshaji wa bandari, mamlaka za forodha, mamlaka za udhibiti wa bidhaa zinazoingia bandarini, kampuni za utoaji wa mizigo na mamlaka zinazohusika na ulinzi na usalama bandarini kuwa tayari kutekeleza mpango huu kwa vitendo kufikia malengo yake.

“Unapokuwa na ufanisi wa bandari ambayo ndiyo mlango mkuu wa uchumi bila shaka athari zake zinakuwa kubwa zaidi, kwa hiyo tusiishie kutia saini tuhakikishe tunayatekeleza haya,” amesema.

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Dk Khalid Mohamed Salim amesema Bandari ya Malindi ni ndogo, ilijengwa mwaka 1920 na wakati huo idadi ya wananchi walikuwa wacheche na mahitaji yalikuwa madogo lakini kwa sasa kila kitu kinaongezeka.

Dk Khalid amesema kipindi cha nyuma kumekuwapo msongamano mkubwa, vifaa vicheche, taaluma ndogo na malalamiko mengi, meli zilikuwa zikichelewa zikikaa nangani kwa zaidi ya siku 32 katika Bandari ya Malindi.

“Kutokana na hali hiyo, wapo baadhi ya watu waliamua kutoleta meli zao Zanzibar na kuzipeleka Mombasa, Kenya nyingine kwenda Dar es Salaam, huku bei ya kuleta makontena Zanzibar ilikuwa kubwa hivyo hali ya maisha ilipanda sana,” amesema.

Amesema baada ya Serikali kuanza kuchukua hatua za kufanya maboresho ya bandari hiyo na kumpa mwendeshaji kampuni ya kigeni kutoka Ufaransa ya AGL, kupitia kampuni tanzu ya Zanzibar Multpurpose Terminal (ZMT) takribani Dola 80 milioni za Marekani (Sh212 bilioni) zimeokolewa.

Amesema fedha hizo zilikuwa zinatumika nje ya Zanzibar kuhudumia usafiri wa makontena na kukaa meli muda mrefu katika Bandari ya Malindi.

“Lakini katika kuongeza ufanisi wa bandari, Rais aliagiza kushirikiana na Taasisi ya Tony Blair kuandaa mpango wa maboresho wa huduma za bandari ambao umeshirikisha wadau wote, zikiwemo kampuni za meli za kigeni za wazawa na watu wa forodha,” amesema.

Amesema mpango huo umeshirikisha watu wote na wameweka viashiria vya utekelezaji mzuri ambao utakuwa na maeneo ya maboresho katika huduma za bandari kwa upande wa baharini na huduma za bandari baada ya meli kufika nangani na kupata ukuta isikae zaidi ya siku tatu, huku ushushaji na upandishaji wa makontena kwa meli kubwa mzunguko wake uwe chini.

Katika kuleta ufanisi zaidi, Dk Khalid amesema wataunda kamati itakayowashirikisha wadau wote watakuwa wakikutana kila baada ya miezi mitatu, miezi sita na mwaka mmoja ambao unakuwa wa kuangalia ufanisi wa jumla.

Mkurugenzi wa Shirika la Bandari Zanzibar (ZPC), Akif Ali Khamis amesema wataboresha maeneo makubwa manne ambayo ni kuona namna gani ukuta unatumika katika utoaji wa huduma na namna ya kuboresha ufanisi katika kutoa huduma ndani ya saa moja, hivyo kupunguza gharama kwa kadri meli inavyokaa nangani.

Katibu Mkuu wa Mawakala wa Forodha Zanzibar, Ahmed Nassor amesema mpango huo utaondoa changamoto zilizokuwa zinaikumba bandari hiyo.

“Mategemeo yetu ikiwa watashirikishwa wadau wote italeta mafaniko makubwa katika bandari hasa katika eneo la ufungaji na ushushaji wa mizigo, sisi tumeona kutoka makontena saba kwa saa hadi kufika makontena 17 kwa sasa, si kazi ndogo,” amesema.Continue Reading