Simulizi ya padri aliyepanda miti zaidi ya milioni 1.7 katika miaka 65

Mwanza. “Tangu nimeanza kupanda miti mwaka 1959 nikiwa darasa la kwanza mpaka sasa nimepanda zaidi ya miti 1,700,000 kiasi kwamba sasa kila ninapokwenda huwa nakutana na watu wananiambia huu ni mti wangu nilipanda.”

Hayo ni maneno ya Padri wa Kanisa la Katoliki Jimbo la Geita, Thomas Bilingi wakati akisimulia namna alivyopanda miti zaidi ya 1,700,000 katika kipindi cha miaka 65.

Akizungumza na Mwananchi leo Disemba 7, 2024 baada ya kufanya matembezi ya kuhamasisha watu kutumia nishati safi jijini Mwanza, Padri Bilingi mwenye miaka 76 sasa, amesema alivutiwa kuanza kupanda miti baada ya kubaini miti ya matunda huleta ujirani mwema.

“Tangu kuzaliwa kwangu nyumbani nilikuta kuna mti wa matunda ambao kwa kilugha chetu unaitwa Sungwi, sasa watoto wa majirani walikuwa wakija nyumbani kula matunda hayo, nikaona kumbe miti ya matunda inaleta ujirani mwema na huduma mbalimbali,” amesema.

“Nilianza kupanda miti nikiwa na umri wa miaka 11 wakati naingia darasa la kwanza, mwaka 1959, katika shule ya msingi Kasisa iliyopo Buchosa, Mwanza, nikaja kuendelea nikiwa darasa la tano ambapo hapo nilianza kupanda miti kwa wingi,” ameongeza.

Padri Bilingi amesema miti hiyo ameipanda katika maeneo mbalimbali ambayo amekuwa akipita, mfano kwenye taasisi za elimu, dini, Serikali na maeneo binafsi.

“Baadhi ya shule nilizowahi kupanda miti ni shule ya msingi Kasisa, St Ambrose Mitere baada ya hapo nikaenda Nsumba sekondari, kila sehemu nilipokuwa naenda nilikuwa napanda miti na mara nyingi nilikuwa peke yangu, japo baadaye niliamua kushirikisha wenzangu tukawa kama kikundi nikishirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu (TFS),” amesema.

Ameongeza: “Changamoto kubwa ambayo nilikuwa nikikumbana nayo ni kuchekwa, uharibifu wakati mwingine mifugo inapelekwa kwenye maeneo ambayo nimepanda miti. Changamoto nyingine ni wizi, japo hii wakati mwingine nilikuwa na furahia kwamba kama wanaiba mti ina maana anaenda kupanda nyumbani kwake, kitu ambacho ni kizuri,” amesema.

Hata hivyo, amesema mbali na kupanda miti, pia, huwa anahamasisha watu kupanda kupitia mahubiri, mafundisho na kuongea na mtu binafsi akiwaeleza umuhimu wake.

“Nikiwa nafundisha mfano leo Jumamosi, nina vipindi vya ndoa kanisani huwa nawapatia mti na kuwaambia wakapande, endapo ikitokea mti huo ukakauka basi na ndoa yao itakuwa imeishia hapo, huwa wanakuja wananiambia ndoa haijavunjika na mti wenyewe haujakauka,” amesema Padri Bilingi.

Kiongozi huyo wa kiroho amesema moja ya siri ya kuendelea kuwa hai mpaka sasa,ni kutokana na yeye kupanda miti ambayo inamsaidia kiafya na wakati mwingine kujitibu.

“Kupanda miti ipo kwenye damu ndio maana kuna muda huwa nakula majani ya miti hiyo kwa sababu inanisaidia kusafisha na kutibu kifua, mfano badala ya kutumia majani ya dukani mimi nachuma majani ya mti wa mchachai, nakunywa,” amesema.

Akizungumzia maisha ya padri huyo, mmoja wa wadau wa mazingira jijini Mwanza, William Missanga, mbali na kumpongeza amesema kwake kama kijana inamtia nguvu ya kuendelea kupambana kuhakikisha jamii inaondokana na matumizi ya nishati chafu, huku suala la upandaji miti akilipa kipaumbele.

“Ni jambo la kusisimua kwa mimi kama kijana, linanifunza mambo mengi na kunifanya nione bado dunia inanitaka. Bado nina safari ndefu ya kufikia rekodi ya mtu kama huyo kwa sababu sio jambo la kawaida linahitaji kujituma na kuwa moyo,” amesema Missanga.

Balozi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais ambaye pia ni Mkurugenzi wa Taasisi ya MR Tree Foundation, Mrisho Mabanzo (Mr Tree) amesema siku 10 zilizopita amempoteza mama yake, chanzo kikiwa ni moshi uliokuwa unatokana na matumizi ya kuni na mkaa.

“Mama yangu alikuwa mfanyabiashara mkubwa sana wa mkaa mpaka ikawa inafikia wakati analipia miti ili kukata na kupata kuni, lakini madhara yake miaka 30 mbele tumejikuta tunatumia gharama kubwa kumtibu mpaka kumpoteza kwa sababu ya athari zilizobainika kuwa zimetokana na matumizi ya nishati isiyo salama kwa maana ya moshi wa kuni na mkaa,” amesema Mr Tree.

Akizungumzia takwimu, Mr Tree Amesema: “Asilimia 16 ya ardhi ya Tanzania imeelekea kuwa jangwa, zaidi ya ekari 469,000 zinaharibiwa kila mwaka kutokana na matumizi ya kibinadamu hasa matumizi ya kuni na mkaa, hivyo ni viashiria vinatuonyesha hali ya hatari ndiyo maana hali ya hewa haitabiriki.”

Askari mhifadhi misitu kutoka Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) Kanda ya Ziwa, Maija Mkomwa amewataka wananchi kufika kwenye ofisi zao kwa ajili ya kujipatia miti bure ya matunda ya kupanda, huku akihimiza jamii kuachana na nishati chafu.

“TFS tunatoa wito kwa wananchi kwanza kutumia nishati safi kwa maana ya umeme na gesi lakini pia waondokane na nishati zinazoleta uharibifu wa mazingira, mfano kuni na mkaa,. Pia wananchi wapande miti kwa wingi kwa ajili ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi,” amesema Mkomwa.

Naye Mkurugenzi wa Watengenezaji wa KuniSmart na JikoSmart kutoka kampuni ya Chabri Energy, Bernard Makachia ametoa wito kwa kampuni za gesi kupunguza gharama za mitungi ya gesi ili kuwawezesha Watanzania wengi kumudu kununua.Continue Reading

Sababu tatu zachangia kuua mamia ya vichanga Mwanza

Mwanza. Zaidi ya watoto wachanga 1,452 walifariki dunia mwaka 2023 mkoani Mwanza huku sababu ya kukosa hewa na maambukizi, zikitajwa kuchangia vifo hivyo.

Akizungumza Novemba 5, 2024 wakati wa uzinduzi wa programu ya utoaji huduma za afya kwa watoto wachanga (NEST360) katika halmashauri tano za Mkoa wa Mwanza, Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa huo, Dk Silas Wambura amesema watoto hao walifia tumboni na wengine kufariki muda mchache baada ya kuzaliwa.

“Na sababu kubwa zinazochangia watoto hawa kufariki ni kukosa hewa, maambukizi na wakati mwingine wajawazito wanakuja wamechelewa kwenye vituo wakati wa kujifungua na wakati mwingine wanakuja vituo vya afya wakiwa wametumia dawa za kienyeji kuongeza uchungu,” amesema Dk Marwa.

Ameongeza kuwa wajawazito hao wanatumia dawa za kienyeji ili kuharakisha uchungu, hivyo dawa hizo zinawaathiri watoto wakiwa tumboni na wengine kufariki muda mfupi baada ya kuzaliwa.

“Na wakati mwingine hizo dawa zinasababisha kizazi kuchanika na kuhatarisha uhai wa mtoto kabla hajazaliwa, wakati mwingine ni maambukizi kwa sababu wanapotumia hizo dawa wengine wanaziweka ukeni, zile dawa zinaleta maambukizi yanayoweza kuwapata watoto wanapozaliwa na kufariki muda mfupi baada ya kuzaliwa,” ameeleza Dk Marwa.

Dk Marwa amewataka wajawazito kuwahi vituo vya afya wanapohisi dalili za uchungu kwa kuwa kuchelewa kwao husababisha wakati mwingine mtoto kumeza maji ya tumboni na kukisababishia kichanga kupata shida ya upumuaji.

“Mtoto asipopata huduma ya haraka anaweza kufariki kwa sababu mfumo wake wa kupumua una changamoto, kwa hiyo mpango huu utasaidia kuondokana na vifo hivi kwa sababu kwanza utawajengea uwezo watumishi wetu, pili utatusaidia kununua vifaa na vifaa tiba ambavyo kwa maeneo mengine bado ni changamoto,” amesema.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkazi wa NEST360 nchini, Dk Mariam Johari zaidi ya asilimia 80 ya watoto huzaliwa hospitalini, lakini bado watoto milioni 2.3 hufariki kila mwaka duniani.

“Asilimia 80 ya vifo hivi vinaweza kuzuilika. Tanzania imechukua hatua kubwa ya kupunguza vifo vya watoto wachanga ambavyo kwa mwaka 2004/5 vilikuwa vifo 32 kwa kila vizazi hai 1,000 na kupungua hadi vifo 24 kwa kila vizazi hai 1,000 mwaka 2002. Ili kufikia lengo la Maendeleo Endelevu la kuwa na vifo vya watoto wachanga visivyopungua 12 kwa kila vizazi hai 1,000 ifikapo mwaka 2030, Tanzania inapaswa kuimarisha juhudi zake,” amesema Dk Mariam.

Amesema awamu ya kwanza mpango huo ulitekelezwa mkoani Dar es Salaam, Mbeya na Kilimanjaro ambapo vitengo vya huduma za watoto wachanga vilipanuliwa, kutoa vifaa muhimu vya huduma, pamoja na kuwajengea uwezo wahudumu wa afya, awamu ya pili Zanzibar na Mwanza zikiongezwa.

“Katika awamu ya Pili nchini Tanzania, NEST360 imewekeza dola milioni 7.1 kusaidia juhudi za Serikali za kupunguza vifo vya watoto wachanga. Ufadhili huu utazinufaisha moja kwa moja hospitali 28. Hospitali 25 kati ya hizo ni katika mikoa minne ya Tanzania Bara na hospitali tatu Zanzibar,” amesema Dk Johari.

Amesema mpango huo unahusisha ukarabati miundombinu, ununuzi na utoaji wa vifaatiba, kujenga uwezo kwa madaktari na wahandisi wa vifaatiba ili kutoa huduma bora.

Akizindua mpango huo wa miaka minne kuanzia 2024 hadi 2028 katika Halmashauri za Buchosa, Sengerema, Misungwi, Nyamagana na Ilemala, Kaimu Katibu Tawala mkoani Mwanza, Chagu Nghoma amewataka wataalamu wa afya kutumia utaalamu wao ipasavyo kudhibiti vifo vya watoto wachanga.Continue Reading

Wajiolojia wataka bodi ya usajili

Chama cha Jiolojia Tanzania (TGS) kimeitaka Serikali kuharakisha uanzishwaji wa bodi ya usajili wa wataalamu wa jiolojia wa Tanzania, kikisisitiza umuhimu wake katika kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu ya sekta ya madini yaliyoainishwa kwenye Dira ya Maendeleo ya 2030 ya Tanzania.Continue Reading

Samia asema atatafutwa mrithi wa Dk Ndugulile WHO

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema nafasi ya aliyekuwa Mkurugenzi mteule wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Dk Faustine Ndugulile itaelekezwa kwa Mtanzania mwingine mwenye sifa.

Rais Samia amesema hayo leo Jumatatu Desemba 2, 2024 katika hafla ya kuaga mwili wa Dk Ndugulile, aliyekuwa mbunge wa Kigamboni iliyofanyika viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam.

Dk Ndugulile alifariki dunia Novemba 27, 2024 nchini India alikokuwa akipatiwa matibabu. Mwili wake utazikwa kesho Jumanne, katika makaburi ya Mwongozo, Kigamboni.

Alifikwa na mauti ikiwa imesalia miezi michache kwenda kuanza kutumikia nafasi yake mpya WHO Februari, 2025. Alichaguliwa kwenye nafasi hiyo Agosti 2024, akiweka rekodi ya kuwa Mtanzania na mwana Jumuiya ya Afrika Mashariki wa kwanza.

Katika salamu zake, Rais Samia amesema nchi ilimpata mwakilishi: “Wanadamu tunapanga yetu, lakini Mungu anatupangia, Dk Ndugulile ameiweka nchi pazuri lakini Mungu amechukua kilicho chake.

“Tutaingia tena kwenye mashindano tutatafuta Mtanzania mwenye sifa anayeweza kushindana na ulimwengu, tutaingia tena na tutaweka mtu mwenye sifa ileile kutuwakilisha,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema amepokea salamu nyingi za pole kutoka ndani na nje ya nchi, huku akiwashukuru viongozi waliofika kumuaga Dk Ndugulile hasa kutoka WHO.

“Mengi yamesemwa na tumeyasikia mengi katika mchango wake kwa nchi na duniani, uongozi wake, mchango wake katika taaluma ya tiba na siasa hasa kwa wananchi wa Kigamboni,” amesema.

Rais Samia amesema wajibu wa nchi ni kuimarisha uwakilishi wa Tanzania ndani ya nchi na Afrika hasa katika Shirika la Afya Duniani.

“Katika kuimarisha ushiriki wetu ni azma ya Serikali kuhakikisha sasa Watanzania wabobezi tunaweka kila aina ya nguvu watuwakilishe katika fani za kimataifa.

“Dk Ndugulile alikuwa mwanamajumuia kutokana na imani yake ndicho kilichomsukuma akagombee nafasi hiyo na Serikali ikamuunga mkono tukajaliwa kupata nafasi ile, mwanadamu hupati unachokipata unapata majaliwa,” amesema Samia.

Walichokisema WHO

Awali, Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani WHO Kanda ya Afrika, Dk Matshidiso Moeti amesema Dk Ndugulile alikuwa na maono ya kufanya mageuzi makubwa katika shirika hilo.

Amesema tangu aliposhinda nafasi yake Agosti 2024, alishaanza kuandaa namna atakavyoliongoza Bara la Afrika katika nafasi yake mpya.

Amesema kupitia nafasi yake, tayari alianza kuandaa mambo kadhaa kwa kushirikiana na ofisi yake.

“Alitutembelea mwezi uliopita na alizungumza nasi mambo mengi kuhusu kile atakachokuja kukifanya na mageuzi anayoyataka. Tulijiandaa kufanya vizuri zaidi katika uongozi wake na wengi walijiandaa wakiwemo wafanyakazi na wengine ambao tumekuwa tukifanya nao kazi,” amesema Dk Moeti.

Kwa mujibu wa Dk Moeti, taarifa za kifo cha Dk Ndugulile ziliwashtua si tu ofisi ya WHO Afrika iliyopo Brazzaville DRC Congo, bali katika ofisi kuu za WHO Geneva, Uswisi.

“Leo nimeongozana na viongozi wengi, wakiwemo wakurugenzi wa WHO Afrika, mawaziri wa afya na washirika wengine.

“Baada ya taarifa za kifo, nilipokea meseji nyingi na simu kutoka nchi mbalimbali duniani. Machozi ni ya wengi kuondoka kwa Dk Ndugulile na wengi wameumia kuona kiongozi mwenye maono anaondoka bila kutumikia nafasi yake,” amesema Dk Moeti.

Amesema wakati huu wa majonzi ni kubaki kushangilia maisha yake, kwani ni mtu aliyekuwa na uwezo mkubwa katika afya ya umma na waliamini uwezo wake angeutumia zaidi katika sera za kiafya kuhakikisha analeta mabadiliko Afrika.

Dk Moeti amesema kifo cha Dk Ndugulile kimemtonesha kidonda cha Dk Mwele Malecela.

“Kwa niaba ya WHO natoka pole kwa Tanzania na Serikali ya Tanzania na Rais wa Jamhuri ya Jamhuri ya Tanzania, watoto na mke wake,” amesema Dk Moeti.

Tamsa, MAT wamlilia

Chama cha Madaktari Wanafunzi Tanzania na (Tamsa) na Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) wamesema wataenzi mema aliyoyaacha Dk Ndugulile.

Akisoma salamu za Tamsa, Makamu wa rais wa chama hicho, Dua Almas amesema walizipokea taarifa za kifo cha cha mlezi wao Dk Ndugulile kwa masononekana na wanahisi wamepoteza kioo kuelekea kutimiza ndoto zao.

“Dk Ndugulile alikuwa mwanachama hai na alihudumu nafasi mbalimbali katika chama chetu, ikiwemo katibu mkuu na alipohitimu masomo aliendelea kuwa mwanachama na kutoa michango yake, alikuwa anatupa moyo siku moja tunaweza kufanikiwa zaidi yake,” amesema Almas.

Amesema Dk Ndugulile alikubali kuwa mlezi wa chama hicho tangu 2023 na alikuwa msaada mkubwa, hivo kifo chake ni pigo kwao.

Kwa upande wake, rais mteule wa MAT, Dk Alex Msyoka amesema Dk Ndugulile alikuwa daktari bingwa wa afya ya jamii pamoja na kwamba alikuwa mwanasiasa, hakuweka kando taaluma yake.

“Tutamkumbuka kwa mambo mengi, ikiwemo alipokuwa mstari wa mbele kukabiliana na ugonjwa wa Uviko 19, na alikuwa kinara kwenye kupambana ya maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi,” amesema Dk Msyoka.Continue Reading