Bodi ya Mapato Zanzibar yapandishwa hadhi

Bodi ya Mapato Zanzibar yapandishwa hadhi

Zanzibar.

Baada ya Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) kupandishwa hadhi na kuwa Mamlaka ya Mapato Zanzibar (ZRA), inatarajiwa kuongeza makusanyo ya kodi.

Mbali na makusanyo, pia inategemewa kuimarisha huduma za usimamizi wa kodi na uwajibikaji wa ulipaji kodi kwa hiari.

Kwa kipindi cha miezi sita, inajipanga kukusanya Sh300 bilioni kutoka Sh293 bilioni za awali sawa na wastani wa ukusanyaji wa Sh500 milioni kwa mwezi.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari katika ofisi za mamlaka hiyo Mazizini Mkoa wa Mjini Magharibi leo Ijumaa Januari 13, 2023, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Dk Saada Mkuya amesema mabadiliko hayo yanatarajia kuongeza weledi wa watumishi.

“Ukusanyaji na kuongezeka kwa mapato kunakwenda sambamba na kiwango cha huduma bora kwa wadau na walipa kodi, hivyo kurahisisha ulipaji kodi wa hiari,” amesema.

Sheria namba 11 ya mwaka 2022 ilipitishwa rasmi Desemba 14 na Baraza la Wawakilishi na Desemba 29, 2022 Rais alitia saini na tayari imeshatangazwa katika gazeti la serikali.

Dk Saada amesema sababu za kuanzishwa kwa ZRA ni pamoja na kuwa taasisi imara zaidi ya ukusanyaji mapato na mfumo bora zaidi wa kiutendaji ambao utahakikisha uwajibikaji wa watendaji na mfumo mzuri wa usimamizi.

Kingine ni kutoa taswira ya kuwa na taasisi yenye mamlaka na nguvu kwa walipa kodi na kuondosha mtazamo wa udhaifu kuhusu taasisi hiyo kwa sasa.

Pia ni kujenga taswira ya chombo cha kukusanya kodi kinachoaminika, kuheshimika na kukubalika kwa jamii ndani na nje ya Zanzibar.

“Tunataka mamlaka hii iwebora na inakuwa katika viwango vya kimataifa kuendana sawa na mamlaka zingine katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kwani imepewa majukumu makubwa ya kusimamia mapato ya nchi,” amesema.

Wakati huohuo, Rais wa Zanzibar Dk Hussein Mwinyi amemteua Yussuf Juma Mwenda kuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka hiyo.
Mwenda aliteuliwa kuwa kamishna wa ZRB Machi, 2022 baada ya aliyekuwapo Salum Yussuf Ali uteuzi wake kutenguliwa na Dk Mwinyi.

Mwenda ambaye aliwahi kuwa Meya wa Manispaa ya Kinondoni, wakati anateuliwa kuwa kamishna wa ZRB alikuwa ofisa katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Source: mwananchi.co.tz

Original Media Source

Share this news

Facebook
Twitter
LinkedIn
WhatsApp

This Year’s Most Read News Stories