Wakopaji wanaodhalilishwa mitandaoni wapewa mbinu

Dodoma. Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC) imewataka watu wanaomba mikopo kidijitali, kusoma maelekezo vizuri ili kuepuka kuruhusu kampuni hizo kuingia katika orodha ya namba za simu (phone book) na kuwadhalilisha.

Kauli hiyo imekuja wakati baadhi ya kampuni zinazotoa mikopo kwa njia ya kidijitali, kutuma ujumbe mfupi wa maneno unaodhalilisha na wakati mwingine kutuma picha za vitambulisho vya wanaowadai.

Hatua hiyo imekuwa ikiibua malalamiko kwa jamii na hadi imekuibuliwa bungeni ambapo Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson alionyesha kukerwa na udhalilishaji unaofanywa kwa kuwashirikisha wasiohusika na mikopo hiyo.

Spika Tulia alieleza hayo Juni 27, 2024, bungeni wakati wa kipindi cha maswali na majibu akiitaka Serikali ieleze suala hilo ambalo lilikuwa likijadiliwa zaidi nje ya Bunge, “sijui kama kuna mwongozo wowote na Serikali mnalipokea na mnalifanyia kazi, hilo limekuaje.”

Aliyekuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye alijibu suala hilo akikiri kuwepo kwa changamoto hiyo ya watu ambao wanakopeshana mitandaoni na baadaye wanatuma taarifa kwa watu wanaomzunguka mkopaji.

Nape alisema Serikali imeiagiza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na Kitengo cha Kudhibiti Wizi Mtandaoni na Jeshi la Polisi kulifanyia kazi.

Aprili 1, 2024 Mwananchi iliripoti malalamiko ya baadhi ya watu wanaotumiwa ujumbe wa kuwataka kuwakumbusha waliokopa kulipa madeni yao, na jinsi kampuni zinavyopata namba hizo za simu.

“Ndugu wa karibu/jamaa/rafiki/jirani wa (jina la mkopaji na namba ya simu) aliyechukua mkopo kwa nia ya mtandao kupitia application ya… unafahamishwa kuwa mtu huyu amekiuka makubaliano kwa kutolipa deni siku husika ya marejesho na kutopokea simu za ofisi, hivyo tutamchukulia hatua kwa kosa hilo.

“Unaombwa kumpigia simu muhusika na kumjulisha kuwa ana masaa mawili ya kulipa deni kabla ya hatua kali hazijachukuliwa dhidi yake. Fanya hivyo kuepuka usumbufu.”

Leo Jumatatu, Novemba 25, 2024, Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dk Emmanuel Mkilia akizungumzia maandalizi ya warsha ya kuongeza uelewa kuhusu dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi jijini Dodoma amegusia suala hilo la udhalilishaji.

“Kimsingi tumeona kuna uvunjifu mkubwa wa sheria ya ulinzi wa Taifa, hasa watu wanaotumia mitandao wanapata nafasi kutumia picha na vitambulisho vya watu na wanatumia sms (ujumbe mfupi wa maneno) kwa watu wote walioko ndani ya simu husika hilo ni kosa kisheria,” amesema.

Amesema suala hilo wamekuwa wakilishughulikia kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kuhakikisha taasisi ndogo za fedha ziwe zimesajiliwa kisheria na BoT.

Amesema wanaofanya biashara hiyo wanatakiwa kuzingatia sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi na ndio maana wengi wamefungiwa hivi karibuni kujishughulisha na biashara hiyo.

Amesema mwananchi anapoomba mkopo kupitia programu tumizi ‘application’ hizo kwa kujua ama kwa kutokujua inakuwa ni sharti kama hutalipa deni hilo ambalo wanawataka aruhusu ili waweze kuingia kwenye orodha ya namba za simu (phone book) na kuangalia anwani ya watu unaowasiliana nao.

Dk Mkilia amesema bila kujua mwananchi anapoweka alama ya tiki, application hiyo inakuwa na ruhusa ya kuingia katika orodha ya namba za simu, hivyo hata wakati mwingine kabla ya muda wa kulipa kufika taarifa zinapelekwa za kumkashifu huyo mtu kwa watu wote anawasiliana nao.

“Kuwaasa wananchi kupitia vizuri maelekezo yanayoelekezwa mle ile usijikute kuwa ni mwathirika,” amesema.

Tayari BoT imezifungia kutoa mikopo programu tumizi (application) 69 baada ya kuzibaini zinaendesha shughuli hiyo kidijitali bila kuwa na leseni wala idhini.

BoT ilitangaza uamuzi huo Novemba 21, 2024 kupitia taarifa iliyosainiwa na Gavana wa Bot, Emmanuel Tutuba ikiutahadharisha umma wa Watanzania kutojihusisha na majukwaa na programu tumizi zilizofungiwa.

Kuhusu warsha ya kuongeza uelewa juu ya dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi, Dk Mkilia amesema warsha hiyo itafanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Desemba 17 hadi 18, 2024 ambapo washiriki ni maofisa ulinzi wa taarifa binafsi (DPOs) wa taasisi za umma na binafsi.

Amesema lengo ni kuelimisha wadau wa ulinzi wa taarifa binafsi nchini na kutoa elimu pamoja na maarifa muhimu kwa taasisi za umma na binafsi kuhusu utekelezaji wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ya mwaka 2022 na kanuni zake.

Dk Mkilia amesema katika kutekeleza agizo la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa Aprili 3,2024 wakati akizindua tume hiyo taasisi 700 za umma na binafsi zimejisajili katika tume hiyo.

Mwakilishi wa Kampuni ya Hilton Law Group ambao wanashirikiana na PDPC katika warsha hiyo, Wakili Dorothy Ndazi amesema ni muhimu kwa taasisi zote kuelewa wajibu wao kuhusu dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi.Continue Reading

Zanzibar ilivyojizatiti kuondoa urasimu bandarini

Unguja. Ukizinduliwa mpango wa maboresho ya huduma za bandari, Rais wa Zanzibar , Dk Hussein Mwinyi amesema utaleta mageuzi ya kiutendaji na kuondoa urasimu kwa kupeana majukumu kwa kila anayehusika kupitia viashiria vilivyowekwa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo uliondaliwa na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi kwa kushirikiana na Taasisi ya Tony Blair (TBI) leo Novemba 22, 2024 Ikulu Zanzibar, Rais Mwinyi amezitaka taasisi hizo kuwa tayari kuutekeleza ili ulete tija.

Mpango huo pia unazihusisha wizara tatu za Ujenzi, Biashara na Fedha na taasisi 16.

Dk Mwinyi amesema: “Iwapo kuna mmoja katika mnyororo huo hatimizi wajibu wake, atafanya kazi nzima isiende inavyotakiwa, na itabidi wafanye tathimini kila wakati kupitia viashiria vilivyowekwa na wale ambao watashindwa kutekeleza hilo nitapenda kupata taarifa ili tuchukue hatua stahiki.”

“Endapo taasisi zote zitafanya kama inavyotakiwa hakika tutapata mafanikio makubwa katika nchi yetu, hivi sasa nchi kama za Singapore, Gambia na Kenya wanatumia mfumo huo wa ushirikishwaji na wameweza kupata mafanikio makubwa,” amesema Dk Mwinyi.

Ametaja malengo mengine ya mpango huo ni kurahisiha ushushaji wa makasha, kupunguza muda wa meli kukaa ukutani na kupunguza muda wa meli kukaa nangani, hivyo kupunguza muda wa kutoa mizigo bandarini na kuongeza ukuaji wa uchumi.

Dk Mwinyi amesema Serikali imedhamiria kuendesha huduma za bandari kwa ufanisi zaidi kwa kuzingatia bandari ni mlango mkuu wa uchumi wa nchi.

Amesema mikakati ya Serikali ya ukuzaji uchumi Zanzibar inaendelea kuwawekea wafanyabiashara mazingira mazuri na sasa inatarajia kuanza ujenzi wa bandari jumuishi ya Mangapwani.

“Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote kuendeleza sekta ya bandari nchini na miongoni mwa mipango ni kuimarisha bandari za Malindi, Shumba, Mkoani, Pemba,” amesema.

Amewataa wadau wote zikiwemo kampuni za uendeshaji wa bandari, mamlaka za forodha, mamlaka za udhibiti wa bidhaa zinazoingia bandarini, kampuni za utoaji wa mizigo na mamlaka zinazohusika na ulinzi na usalama bandarini kuwa tayari kutekeleza mpango huu kwa vitendo kufikia malengo yake.

“Unapokuwa na ufanisi wa bandari ambayo ndiyo mlango mkuu wa uchumi bila shaka athari zake zinakuwa kubwa zaidi, kwa hiyo tusiishie kutia saini tuhakikishe tunayatekeleza haya,” amesema.

Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Dk Khalid Mohamed Salim amesema Bandari ya Malindi ni ndogo, ilijengwa mwaka 1920 na wakati huo idadi ya wananchi walikuwa wacheche na mahitaji yalikuwa madogo lakini kwa sasa kila kitu kinaongezeka.

Dk Khalid amesema kipindi cha nyuma kumekuwapo msongamano mkubwa, vifaa vicheche, taaluma ndogo na malalamiko mengi, meli zilikuwa zikichelewa zikikaa nangani kwa zaidi ya siku 32 katika Bandari ya Malindi.

“Kutokana na hali hiyo, wapo baadhi ya watu waliamua kutoleta meli zao Zanzibar na kuzipeleka Mombasa, Kenya nyingine kwenda Dar es Salaam, huku bei ya kuleta makontena Zanzibar ilikuwa kubwa hivyo hali ya maisha ilipanda sana,” amesema.

Amesema baada ya Serikali kuanza kuchukua hatua za kufanya maboresho ya bandari hiyo na kumpa mwendeshaji kampuni ya kigeni kutoka Ufaransa ya AGL, kupitia kampuni tanzu ya Zanzibar Multpurpose Terminal (ZMT) takribani Dola 80 milioni za Marekani (Sh212 bilioni) zimeokolewa.

Amesema fedha hizo zilikuwa zinatumika nje ya Zanzibar kuhudumia usafiri wa makontena na kukaa meli muda mrefu katika Bandari ya Malindi.

“Lakini katika kuongeza ufanisi wa bandari, Rais aliagiza kushirikiana na Taasisi ya Tony Blair kuandaa mpango wa maboresho wa huduma za bandari ambao umeshirikisha wadau wote, zikiwemo kampuni za meli za kigeni za wazawa na watu wa forodha,” amesema.

Amesema mpango huo umeshirikisha watu wote na wameweka viashiria vya utekelezaji mzuri ambao utakuwa na maeneo ya maboresho katika huduma za bandari kwa upande wa baharini na huduma za bandari baada ya meli kufika nangani na kupata ukuta isikae zaidi ya siku tatu, huku ushushaji na upandishaji wa makontena kwa meli kubwa mzunguko wake uwe chini.

Katika kuleta ufanisi zaidi, Dk Khalid amesema wataunda kamati itakayowashirikisha wadau wote watakuwa wakikutana kila baada ya miezi mitatu, miezi sita na mwaka mmoja ambao unakuwa wa kuangalia ufanisi wa jumla.

Mkurugenzi wa Shirika la Bandari Zanzibar (ZPC), Akif Ali Khamis amesema wataboresha maeneo makubwa manne ambayo ni kuona namna gani ukuta unatumika katika utoaji wa huduma na namna ya kuboresha ufanisi katika kutoa huduma ndani ya saa moja, hivyo kupunguza gharama kwa kadri meli inavyokaa nangani.

Katibu Mkuu wa Mawakala wa Forodha Zanzibar, Ahmed Nassor amesema mpango huo utaondoa changamoto zilizokuwa zinaikumba bandari hiyo.

“Mategemeo yetu ikiwa watashirikishwa wadau wote italeta mafaniko makubwa katika bandari hasa katika eneo la ufungaji na ushushaji wa mizigo, sisi tumeona kutoka makontena saba kwa saa hadi kufika makontena 17 kwa sasa, si kazi ndogo,” amesema.Continue Reading